7/31/2004

UNAIONAJE ADHABU HII?

Mwanamke aliyekamatwa akiiba petroli (ambayo hapa Marekani huitwa gesi) ya thamani ya dola 4 na senti 52, aliamriwa na mahakama kusimama nje ya kituo hicho cha petroli na bango kubwa mbele ya kifua chake lisemalo: NILIKAMATWA NIKIIBA PETROLI.
Watu walijaa hapo kituoni kumuona na wengine walipeleka watoto wao ili wajifunze ubaya wa wizi. Bonyeza hapa utazame picha yake na habari yenyewe.

7/29/2004

MAKALA

Inaelekea bado tatizo la tovuti/ webu ambako ndiko ninahifadhi makala zangu liko pale pale. Ninaomba samahani tena. Nimepata barua pepe za wale wanaolalamika kuwa wanapokongoli ziliko makala hawapati kitu. Ni kweli. Kuna tatizo. Ninajitahidi kusawazisha.


7/28/2004

UNYAMA, UNYAMA...MUNGU MKUBWA!

Jina la Mungu limetumiwa miaka nenda rudi kuhalalisha unyama. Mwizi wa kura George Bush na wahafidhina wenzake wanadai kuwa vita wanavyoviongoza dhidi ya "ugaidi" ni vita ya wenye Mungu wa kweli dhidi ya wafuasi wa shetani. Makundi yanayojiita kuwa ni ya kiislamu nayo yanafanya unyama dhidi ya wengi wasio na hatia kwa madai kuwa wanapigana vita vya kidini. Wanampigania Mungu wa kweli! Mwanazuoni mmoja, jina limenitoka, aliwahi kusema kuwa dunia ina dini za kutosha kutufanya tuuane, tugombane, na kuchukiana lakini hakuna dini za kutufanya tuishi kama ndugu.

Tazama picha hii ya unyama usio na mfano uliofanya dhidi ya Mmarekani Nick Berg. Napenda kukutaarifu kuwa picha hii, hasa mwishoni, inatisha na kuchafua roho kabisa. Kama una roho nyepesi nakushauri usiitazame. Kongoli hapa uione.


7/27/2004

SHAYO NA GODLISTEN

Kwanza kabisa poleni. Kisha karibuni ndani! Toka kupambana na Mwalimu Sango hadi kupambana na Rais Kichaka!

7/26/2004

Saddam Hussein ni Mshairi!

Imeelezwa kuwa Saddam Hussein anatumia muda wake jela kuandika mashairi. Moja ya mashairi yake linamhusu dikteta mwenzake aitwaye George Bush. Pia anapenda sana kutengeneza bustani. Taarifa zinasema kuwa anapenda kula mkate wa Kimarekani uitwao Muffins, na biskuti. Kongoli hapa usome habari nzima. Sijui kama unajua kuwa Saddam ni mtunzi pia wa vitabu. Ameshaandika vitabu vitatu: Zabibah and the King, The Fortified Castle and Men and the City, na Be Gone Demons! Vitabu hivi vilichapwa bila jina la mtunzi. Kongoli hapa usome zaidi.

Kitendawili...

Tuenzi vitendawili.
Nani anaweza kutegua kitendawili hili?

Kitendawili...
Msichana wangu amejishika kiuno.

Una jibu? Niandikie.



Oya, Shika Mchuma!

Ninapitia vitabu vyangu vya kumbukumbu nilizoandika nikiwa Tanzania. Hii ni sehemu ndogo ya mambo niliyoandika katika pilikapilika za kwenye daladala katika jiji la Dar Es Salaam. Ni kati ya mwaka 1999-2001.

Oya, Shika Mchuma!

Kondakta: Kaa mkao wa pesa.
Abiria: Si tumetosha? Twende basi!

Kondakta: Tunafanya kazi kwa hesabu mama mdogo.
Abiria: Hebu twendeni. Kuna watu huko mbele.
Kondakta: Kama una haraka ungeenda toka juzi. Tuko kazini hapa.
Mpiga debe: Wenye haraka wanaonyesha. Wenye haraka huchukua teksi.
Abiria: Tukichukua teksi mtakula wapi. Hebu acheni dharau. Twendeni, gari si imejaa?
Mpiga debe: Jamani, mchuma haujai. Inayojaa ni ndoo ya maji. Haya, Kariakoo, Kariakoo... gari nyeupe hii.
 
XXXXXXXXXXXXXXX****XXXXXXXXXXXXXXXXXXX
 
Kondakta: Tiketi mbele kama tai. Tiketi mbele jamani. Tiketi sio mzigo wa bangi...mbele kama tai.
 
XXXXXXXXXXXXXX***XXXXXXXXXXXXXXXXXXXXX
 
Kondakta: Manzese wapo?
Abiria: Tupooooo...
Kondakta (akijifanya kuwa hakusikia): Manzese hakuna sio?
Abiria (kwa hamaki): Shushaaaaa...Tupo!
Kondakta (huku akijizuia kucheka): Babu endesha, Manzese hakuna.
Abiria: He, we konda vipi? Tumesema tupo!
 
XXXXXXXXXXXXX***XXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXX
 
Ni saa tano usiku. Siku ya jumamosi. Kituo cha mabasi Mwenge. Tunaelekea Mbezi Beach.
 
Abiria: Dereva twende bwana...saa za majeruhi hizi.
Kondakta: Bado vichwa babu. Gari haiendi mswaki hii hata siku moja.
Abiria (amelewa chakari): Nina haraka ya kufumania. Nimeambiwa saa tano na nusu ndio saa ya kumfumania mbaya wangu.
 
Mara abiria huyu aliyelewa anaanza kutapika.
 
Abiria 1: Jamani watu wameanza kutapika humu ndani.
Abiria 2: Nipisheni nitoke miye...
Abiria 3: Afadhali niende kwa miguu.
Kondakta: Kuna wagonjwa huku?
Abiria 4: Twendeni. Hamjui ni mambo ya wikiendi haya?
Abiria 5: Pombe za bure hizo.
Kondakta: Kama sio pombe za bure basi ni za mkopo. Shuka bwana mzee. Walevi hawa kwanza huwa hawataki kulipa.
 
XXXXXXXXXXXXXXXX***XXXXXXXXXXXXXXXXXXX
 
Abiria: Kuna nafasi?
Kondakta: Nafasi kwani gesti hapa? Kama unakwenda, twende.
 
XXXXXXXXXXXXXXX***XXXXXXXXXXXXXXXXXXXX


 


Mabadiliko...

Kutakuwa na mabadiliko ya muundo na rangi ya blogu hii siku za karibuni. Mpangilio wa kila kitu utakuwa tofauti. Ila blogu itakuwa "rafiki wa watumiaji" kuliko ilivyo hivi sasa. 

7/23/2004

Wanablogu ni Waandishi?

Bado mjadala huu haujatuama. Je wanablogu (bloggers) ni waandishi wa habari? Je blogu ni uandishi? Waandishi, wanasiasa, watengeneza sera, wanataaluma, n.k. wana mawazo tofauti juu ya blogu. Wako wanaosema kuwa wanablogu (bloggers) ni aina fulani ya waandishi. Wengine wanasema hapana. Lakini kukubaliwa kwa wanablogu kuhudhuria mkutano wa chama cha Demokrasia cha hapa Marikani, ambao utampitisha John Kerry na John Edwards kuwa wagombea Urais na mgombea mwenza, kumechukuliwa kama ni moja ya hatua ambazo zinawapa wanablogu hadhi ya uandishi.

Kwa Wale Walioko Marikani

Kama hujatazama sinema mpya ya Michael Moore : Fahrenheit 911, tafadhali sana nenda kaitazame. Pia tazama filamu zake nyingine hasa Bowling For Columbine na Roger and Me. Nenda kaitazame, utakuja kuniambia! Wale walioko Tanzania, kuna kundi la vijana wenye mwamko wa kimapinduzi ambao watakuwa na kopi yake siku za karibuni. Nitatoa maelezo ya jinsi ya kuwapata.




SITAOMBA MSAMAHA...

"Sitaomba msamaha." Haya ni maneno ya Rais wa Ufilipino, mwanamama Gloria Arroyo, kufuatia kuondoa majeshi ya nchi yake toka Iraki ili kuokoa maisha ya Angelo de la Cruz aliyekuwa ameshikiliwa mateka huko Iraki. Arroyo anasema kuwa Angelo ana familia ya watoto tisa wanaomhitaji hivyo uhai wake ndio kipaumbele cha nchi yake. Serikali ya Rais Kichaka (Bush) imetoa malalamiko juu ya hatua hiyo.

Tujiulize: Hivi binti yake Bush angekuwa ameshikiliwa na hao jamaa na wakiwa wanatishia kumkata kichwa, Bush angesema, "Potelea mbali. Wamuue. Siwezi kutimiza masharti ya magaidi. Nafuu mtoto wangu auawe kikatili kuliko kuwasikiliza. " Angethubutu kusema hivyo? Thubutu!


SAMAHANI SANA (MAKALA ZANGU)

Ndugu zanguni, kuna tatizo kidogo kwenye "link" za makala zangu. Ninarekebisha. Kwahiyo baada ya muda mfupi mtaweza kupata makala ninazotoa kwenye gazeti la Mwananchi kila jumapili. Na pia makala nyingine nilizoandika huko nyuma kwenye magazeti mengine. Na tafsiri ya zile nilizoandika kwa kiswahili. Ninaomba mniwie radhi kwa usumbufu. Makala unayoweza kuipata ni moja iitwayo BABU SEYA. Hii ilitoka jumapili mbili zilizopita.


Kenya Wanatufundisha Nini?

Baada ya wapinzani kumtoa madarakani dikteta aliyekalia kiti toka mwaka 1979, Mzee Moi, wapinzani wa Tanzania walitumia nafasi hiyo kuwataka wananchi wakatae chama tawala na kuleta mabadiliko. Kama Kenya ndio mfano ambao viongozi wa upinzani Tanzania wanataka wananchi wauige, basi huu ni mfano mbaya sana. Kenya inatupa fundisho moja kubwa sana. Vyama vya siasa vinaongozwa na binadamu. Viwe ni vyama vya upinzania au chama tawala. Wezi wa chama cha KANU hawakuwa wakiiba eti kwakuwa wao ni wanachama wa KANU. Waliiba kwa kuwa ni wanadamu ambao hawana maadili na utu. Ubinadamu wa viongozi wa upinzania hauna tofauti na ubinadamu wa viongozi wa chama tawala. Tunaona jinsi ambavyo viongozi waliokuwa wakidai kuwa katiba ya Kenya ibadilishwe, sasa wameingia madarakani wamebadili msimamo. Tumeona kashfa za rushwa zinawaandama kila kukicha. Leo hii gazeti la Daily Nation lina habari hii ya Waziri wa Uchukuzi ambaye inaelekea kapewa kitu kidogo na Wachina. Umeusikia wimbo wa Wainaina  uitwao Kenya Nchi ya Kitu Kidogo? Anasema, "askari kama unataka chai nenda Limuru: Limiru inalimwa chai. Kenya ni nchi ya kitu kidogo wakati wa "baba" Moi. Ni nchi ya kitu kidogo wakati wa Mzee Kibaki. Halafu unaona nchi zetu za Afrika, badala ya ku-recycle takataka, tuna-recycle watawala.













Utata wa ndoa Marekani

Wabunge wenye siasa za kihafidhina wameshindwa kupitisha sheria ambayo ingeifanya katiba ibadilishwe ili kutamka kuwa ndoa ni kati ya mwaume na mwanamke! Rais Bush na chama cha Republican wamekuwa mstari wa mbele kutafuta njia ya kuzuia kisheria kasi ya ndoa za wanaume kwa wanaume na wanawake kwa wanawake. Swali ambalo Bush na wenzake wanashindwa kujibu hadi hivi sasa ni hili: kwanini wanataka kubadili katiba kwa kutumia imani zao za kidini?
Bush na wenzake wanadai kuwa ndoa mwanaume na mwanamke ndio mapenzi ya Mungu. Sasa kama je mtu hamwamini huyo Mungu wao? Hili suala kwa kifupi ni gumu sana. Huko Afrika Kusini kipindi cha luninga cha Yizo Yizo kimeonyesha wanaume wawili wakipigana busu kwa mapenzi na mahaba yasiyo na kifani. Ni mara ya kwanza kwa luninga nchini humo kuonyesha picha ya namna hii. Afrika Kusini ndio nchi pekee Afrika hivi sasa ambayo katiba yake inatoa haki kwa watu wa jinsia moja kuwa na mahusiano ya kimapenzi.

7/21/2004

Jifunze Kiswahili

Jifunze kiswahili:
Genetic engineering= uhandisi wa maumbile
Biodiversity= bioanuai
Cloning= kupachiza
Hacker= mchazaji
DNA= shanga za urathi
Stem cells= seli asili

UJUMBE KWA "CRITIC"

Ndugu yangu uliyetuma maoni yako kwa jina la CRITIC, tafadhali sana nitumie anuani yako. Nadhani uko New York. Umezungumzia juu ya Taifa la Waislamu. Ningependa kuwa na anuani yako ili tuendeleze mjadala. Pia kuhusu blog kwa kiswahili, nadhani itaitwa blogu. Kwahiyo weblog itakuwa webulogu au tovutiblogu.


Narudia Shairi

Narudia kuweka tena sehemu ya shairi langu liitwalo "Utamaduni Msalabani." Wengi wametaka niweke sehemu nzima. NItafanya hivyo karibuni. NItarudia sehemu niliyoweka mwezi uliopita. Nataka usome na utafakari sana mistari hii michache.

Utamaduni Msalabani
Kura twapiga,
Sadaka twatoa,
Kodi twalipa,
swala twasali,
Walalanjaa Cha moto,
mbona
Bado twakiona?
 
Demokrasia ghasia
Mafukara twauziwa,
Jehanamu ya moto
Masikini twatishiwa,
Wa kusema wamesema
Wa kusikia ni viziwi,
Hivi chukua chako mapema
Ni azimio la wapi?
                                         - Dar Es Salaam, Tanzania 2003

7/20/2004

Yesu Anakuja!

Bado ninaendelea kukumbana na watu wanaohubiri kuwa Yesu yu karibu kuja. Mimi siwaelewi kabisa. Ninavyoelewa mimi ni kuwa Yesu yu karibu aondoke. Yuko nasi toka siku nyingi ila hatujui. Sijui tunasubiri ashuke toka mawinguni. Unajua asilimia 90 ya mambo ambayo Yesu aliyasema yalikuwa ni mafumbo. Usipoweza kufumbua, utabaki ukimsubiri. Kwanza watu wengi wanaomhubiri Yesu, hawamfahamu Yesu sawasawa. Yesu ninayemjua mimi akija leo hii hatakwenda kanisani wala msikitini. Akafanye nini? Watu wake hawako huko! Wakristo na waislamu wanabaki kushikana makoo, "Yesu hakusulubiwa," "Yesu mwana wa Mungu," "Yesu alikuwa ni muislamu," "Yesu alimwaga damu ya ukombozi." Yesu, Yesu, Yesu.... Akija wala hatapoteza muda huko. Atawaacha waendelee na ibada na swala zao na mihadhara na ma-crusade.
 
Kila mara ninaahirisha makala ninayotaka kuandika juu ya hili jambo. Ninahitaji makala ili nichambue vizuri na kufafanua nina maana gani ninaposema kuwa Yesu karibu aondoke. Na kuwa Yesu akitokea Tanzania leo hii hatakwenda kanisani wala msikitini. Watamsikia kwenye "bomba"!

7/18/2004

Shairi: Warsha, mikutano....

SAHAU KABLA YA ALFAJIRI !
La mgambo limelia
wa kusikia wamesikia,
kama ni Ukimwi, haya
kama ni wanawake, haya
kama ni utandawizi, haya
kama ni watoto, haya,
ili mradi una ishu
inayokubalika
kwa wafadhili.
 
Usijali.
 
Mikutano
warsha
makongamano
semina
vikao
utafiti
mafunzo....
 
Tukutane
tuongee
tulalamike
tuonye
tushauri
tukemee
tunywe chai, kahawa
mlo wa mchana
mshiko tushike
picha tupige
tuondoke
tusahau yote kabla ya alfajiri. 
 
Mla kesho ni mla leo.    
                                         - July 18, 2004, Toledo, OH
 

7/13/2004

Mwalimu Nyerere na Benki ya Dunia

Mwaka 1999 Ikaweba Bunting alifanya mahojiano na Mwalimu Nyerere. Mahojiano hayo yalitolewa katika gazeti la New Internationalist. Nimependa sana jibu lake hili. Soma mwenyewe:

I was in Washington last year. At the World Bank the first question they asked me was `how did you fail?' I responded that we took over a country with 85 per cent of its adult population illiterate. The British ruled us for 43 years. When they left, there were 2 trained engineers and 12 doctors. This is the country we inherited.

When I stepped down there was 91-per-cent literacy and nearly every child was in school. We trained thousands of engineers and doctors and teachers.

In 1988 Tanzania's per-capita income was $280. Now, in 1998, it is $140. So I asked the World Bank people what went wrong. Because for the last ten years Tanzania has been signing on the dotted line and doing everything the IMF and the World Bank wanted. Enrolment in school has plummeted to 63 per cent and conditions in health and other social services have deteriorated. I asked them again: `what went wrong?' These people just sat there looking at me. Then they asked what could they do? I told them have some humility. Humility - they are so arrogant!

Ndio Mwalimu huyo. Ukitaka mahojiano kamili kongoli hapa.
Ukitaka kusikiliza hotuba za Mwalimu Nyerere nenda hapa.

7/12/2004

Babu Seya

Itabidi nifanye nifafanue kidogo juu ya mawazo yangu kuhusu suala la Babu Seya. Nimepata barua pepe nyingi. Baadhi zinaonyesha kuwa hoja yangu ya msingi haikueleweka. Nitatoa ufafanuzi baadaye ndani ya blogu hii. Na pengine kwenye makala ya jumapili. Rudi baadaye. Ninakwenda nyumbani kupumzika. Kwahiyo baadaye. Uhuru!

7/11/2004

Swahili becomes AU official language

The African Union has adopted Swahili as its official language. The president of Mozambique, Joachim Chissano, became the first african elder to use African language while in conversation with other African elders. OAU, AU predecessor, used arabic, english, french, and portuguese. Read more...

7/10/2004

TECHNOLOGY AND GOVERNANCE IN TANZANIA

The government of Tanzania goes digital.Read...

ugali na mihogo

Leo mchana na usiku nimekula ugali wa nguvu. Kesho au keshokutwa lazima nijichane kwa mihogo. Chakula cha Tanzania ukiwa Ughaibuni kinakuwa na utamu mara mia zaidi. Jamani sisi tuna chakula kizuri sana. Naona kuna watu wanaona ufahari kukimbilia hivi vyakula vya "kuchukua" (take away)au vyakula vya hoteli kubwa, ambavyo majina yake ukitamka unaweza kuvunja jino, wakidhani kuwa ndio moja ya alama za maendeleo. Wapi! Kama unaona kuwa kula ugali wa kisamvu na nazi na parachichi ni kuwa nyuma kimaendeleo, unahitaji dawa ya kutibu ugonjwa ninaozungumzia kila siku: utumwa wa kimawazo. JIKOMBOE!


Dread Natty Dread! Wazee Maumau wa Kenya wakiwa na nywele zao zinazogusa ardhini. Maumau wakiongozwa na shujaa Dedan Kimathi walikuwa wakisme, "Mzungu arudi Ulaya, Mwafrika apate Tawala." Posted by Hello


Mama Ukweli akikaripia Uovu na Udhalimu! Posted by Hello

UTANYONYESHA AU...?

Mwanamke akiwa na mimba hapa Marekani, kati ya maswali ambayo atakumbana nayo akienda hospitali ni, "Je una mpango wa kunyonyesha au?" Kama umetokea nchi za ulimwengu unaiotwa wa "tatu" utabaki mdomo wazi. Swali hili alipoulizwa Mama Ukweli nilikuwa nikisema, "Kwani mwanamke aliyejifungua anakuwa na maziwa ya nini?" Maziwa ya mama si kwa ajili ya mtoto? Si ndio kanuni ya maumbile hiyo?

Kumbe nilichokuwa sifahamu ni kuwa nchi zinazodaiwa "kuendelea" ni nchi ambazo hazijali afya ya mtoto. Wanawake wanajali kutunza maumbo ya matiti yao. Hawataki kunyonyesha. Asilimia ya wanawake wanaonyonyesha ni ndogo sana. Kunnyonyesha sio tendo linalofanywa hadharani. Ukinyonyesha hadharani watu watakukudolea macho kama vile hazimo.

Wanyama, ukiacha binadamu, wananyonyesha watoto wao. Binadamu ndio viumbe pekee vinavyoamua kuwapa watoto wao maziwa ya wanyama wengine na sio maziwa yao. Na wakati huo huo tunadai kuwa binadamu tumeendelea kuliko ng'ombe au mbuzi. Mbona wao wana busara zaidi yetu kwa kuwapa watoto wao chakula chao?

7/09/2004

Kumbe CIA waongo wakubwa!

Ripoti ya Kamati ya Ujasusi ya Bunge la Marekani imetoa taarifa ambayo imeeleza kuwa shirika la kijasusi la CIA lilitoa taarifa zilizopindishwa na za uongo kuhusu silaha za maangamizi huko Iraki. Shirika hili ambalo lina historia chafu ya mauaji na fitina limeshindwa kupinga ripoti hii. Kwa habari zaidi kongoli (click) HAPA.

7/08/2004

Ushamba Hotelini - 1

Siku moja, mwanzoni nilipowasili hapa, nilikwenda hotelini. Baada ya kuagiza chakula nikaenda zangu kuketi nikisubiri mhudumu aniletee. Nikasubiri. Nikasubiri. Njaa wakati huo inapiga mayowe. Mara akaniambia kuwa chakula changu kiko tayari. Nikajiuliza, "Kama kipo tayari mbona siletewi?" Nikaanza kuhisi kuwa kuna ubaguzi wa rangi. Labda huyu binti mweupe aliyeko kaunta ananichukia kutokana na rangi yangu. Nikaanza kuandaa maneno ya kumpasha. Hakuna kitu kinanchonifurahisha kama kupasha wazungu wabaguzi na kuwatazama wakishika adabu. Wakati nafikiria hivi, akaniita tena kuniambia nikachukue chakula changu. "Unasemaje?" Nikamuuliza. Yaani nimekwenda hotelini na chakula nimelipia anataka nikakibebe mwenyewe? Nikataka kupandisha. Mara nikahisi huenda kuna jambo nisiloelewa. Hivyo nikaamua kwenda kuchukua chakula changu. Lakini shingo upande. Nadhani jambo jingine lililonifanya niache kupandisha ni ukweli kuwa sijaona sehemu ambayo wahudumu wanachukuliwa kama watumwa. Watumwa ambao wanaweza kuitwa kwa namna ambayo hata mbwa akiitwa hatakwenda. Watumwa ambao wanapewa majina ya kuwadhalilisha. Watumwa ambao wakipapaswa na wateja hawana haki ya kulalamika. Wanatakiwa watabasamu. Wavute biashara. Sijaona hiyo bado. Unajua nchi hii ukicheza unajikuta jela au unalipa faini. Sheria mbele!

(KISA HIKI KITAENDELEA, RUDI TENA KUFUATILIA KILICHOTOKEA)

Babu Seya

Suala la Babu Seya linajadiliwa kwenye makala yangu ya kwenye gazeti la Mwananchi jumapili hii. Soma. Nipe maoni yako.

English Soon

Since there are many people who do not speak Swahili and would like to be part of this community, I will start posting in both English and Swahili soon. Uhuru!

7/07/2004

KITWANA CHAUREMBO (Ujumbe wako binafsi)

Wasalaam Kitwana,
TAFADHALI SANA SANA NIPE ANUANI YAKO YA BARUA PPEPE. Unaweza kunitumia hapa: ughaibuni@yahoo.com

Ukimwi na laana toka kwa mungu

Kama ukimwi ni adhabu toka kwa mungu, na malaria nayo ni adhabu? Malaria inaua watu wengi kuliko ukimwi hivi sasa duniani. Ukimwi sio ugonjwa pekee ambao mtu akiupata lazima afariki. Nchi kama Tanzania ina magonjwa mengi sana kama kansa ambayo mtu akipata ni kama ukimwi. Swali ninalotaka kukuuliza ni hili: ni kitu gani kinfanya ukimwi uwe ni adhabu ila sio magonjwa mengine? Na kama ukimwi ni adhabu kutokana na binadamu kuwa na tabia kama za walioishi Sodoma na Gomora, mbona nchi ambazo ukimwi sio tatizo kubwa sana ni zile ambazo hata kwenda kanisani, hekaluni, au msikitini kwa unafiki hawakwendi. Mungu hawamjui hata kidogo. Nchi kama Uholanzi ambako uchangudoa na mapenzi kwa watu wa jinsia moja vimeruhusiwa, idadi ya wenye ukimwi ni ndogo sana.

Kama ukimwi ni adhabu kutokana na uzinzi na uasherati, mbona kuna watu wanaopata ugonjwa huu kutokana na kupewa damu yenye vidudu na sio uzinzi? Na je watoto wanaoambukizwa kutokana na kubakwa? Nchi kama Afrika Kusini kuna imani kuwa mtu mwenye ukimwi akishiriki "tendo la ndoa" na bikira atapona. Hawa watoto wadogo wasio na hatia wanapopata ukimwi wanakuwa wanaadhibiwa kwasababu gani? Kwa makosa ya mababu zao? Inawezekana maana ndivyo Nuhu, ambaye anaheshimiwa sana kwenye Bibilia, alivyofanya. Alikunywa, akalewa, alipochunguliwa na mwanaye Ham, alitoa laana kwa kizazi cha Ham ambacho kilikuwa hakijazaliwa! Mungu wa ajabu kweli huyu. Anaadhibu wasio na hatia. Mbona hawi mfano mzuri? Halfu mungu huyu huyu anakuja kutuambia kuwa ufalme wa mbinguni ni wa watoto.

Mbu wanaweza kuwa wanasaidiana na shetani nini? Si wanatupa malaria???

Klabu ambao wanaume wanakula wakiwa uchi!

Klabu moja hapa Marekani imelazimishwa na mahakama kuruhusu wanawake, ambao kawaida hawaruhusiwi kuingia. Uongozi wa klabu hiyo umedai kuwa hauruhusu wanawake maana mara kwa mara wanaume wanaokwenda katika kilabu hiyo hupenda kula wakiwa uchi! Toba! Soma habari hiyo kwa kirefu HAPA.

7/06/2004

KASHFA KANISA KATOLIKI

Sijui kama unafuatilia kashfa ya kanisa katoliki hapa Marekani. Nimekuwa nikipanga kuandika makala kwa kirefu kwa muda mrefu. Lazima niandike makala hii hivi karibuni. Jumla ya mapadri 4,000 hapa Marekani wanatuhumiwa kujihusisha na vitendo vya ngono hasa na watoto wadogo wa kiume! Soma habari zaidi HAPA
Kutokana na kashfa hiyo dayosisi ya Boston iko hatarini kufilisika kutokana na kudaiwa fidia ya mamilioni na watu waliofanyiwa vitendo vya kinyama na mapandri. Dayosisi ya Portland tayari imetangaza rasmi kuwa imefilisika. Soma habari hiyo HAPA.

7/05/2004

Mapinduzi ya Zanzibar eti ni Uhaini!

Leo nilikuwa natembelea tovuti (website) mbalimbali. Mara nikakumbana na hii tovuti ya huyu bwana anayedai kuwa mapinduzi ya Zanzibar yalikuwa ni uhaini. Na kuwa yote tunayoelezwa juu ya unyama wa utawala wa Waarabu katika kisiwa hiki cha marashi ya karafuu (hivi timu ya KMKM bado iko?) ni uongo mtupu. Habari utaipata ukibonyeza HAPA.

7/03/2004

Babu Seya!

Hii habari kuwa watu wanaandamana kutaka serikali imsamehe Babu Seya na watoto wake kutokana na kifungo cha maisha inanitia kichefuchefu kabisa. Yaani wasamehewe kwakuwa ni waimbaji maarufu? Babu Seya angekuwa ni mlalanjaa Mzee Ramazani na wanaye wa Tandale wamehukumiwa kifungo cha maisha watu wangeandamana? Au mtu maarufu akivunja sheria hapaswi kufungwa? Jela ni ya watu masikini na wasiojulikana sio? Acheni kunikosesha hamu ya chakula!

7/02/2004

Ukipata kikohozi

Usipoteze muda wako kwenda duka la madawa kununua "sumu" ukiwa na kikohozi. Koma kabisa. Unajua asilimia kubwa ya madawa yanayouzwa huko yamejaa sumu. Kwahiyo ukiwa na kikohozi fanya hivi: chukua asali changanya na maji ya uvuguvugu kisha kunywa. Kunywa tani yako. Pia chukua ndimu au limau, changanya na asali, sukari, au sukari guru, kisha kunywa. Pia kama kikohozi kinakusumbua mara kwa mara uwe unakunywa chai ya tangawizi kila mara. Jaribu utaona. Walahi!

7/01/2004


Nje ya Nyumba Ya Sanaa, Morton, jimbo la Washington Posted by Hello

Mzungu...

MZUNGU RUDI ULAYA, MWAFRIKA APATE TAWALA!
KABURU RUDI KWENU, WAZAWA WAPATE TAWALA!
KABURU MATATA IYA!

FREE hit counter and Internet traffic statistics from freestats.com