8/04/2004

Chooni Nairobi!

*Tunaendelea na kitabu changu cha kumbukumbu:

NAIROBI, July, 2003
Tumefika Afrika. Bara langu nilipendalo ambalo huniangusha kila wakati. Kila upande nikilitazama naona maafa. Kama sio vita basi ni ukimwi. Kama sio wizi wa maliasili unaofanywa na kundi la watu waitwao “viongozi” basi ni rushwa, uzembe na uvivu. Kama sio vita vya kugombea dhahabu na almasi basi ni vita vya kikabila. Kama sio wizi wa kura basi ni wizi wa matumaini ya wananchi wa unaofanywa chini ya mwavuli wa ubinafsishaji, soko holela, na utandawizi.

Wakati nasubiri ndege kuelekea Dar Es Salaam toka Nairobi, naelekea chooni. Hapa ndipo ninajua kabisa kuwa nimerudi nyumbani. Baada ya kufungua mlango ambao ulikuwa hauna kitasa na rangi yake imebabuka, nilipigwa kofi kali la harufu nzito iliyokomaa ya mkojo na kinyesi.

Sehemu ya kukojolea, vibao vyake vya marumaru vimebadilika rangi toka rangi nyeupe na kuwa njanonjano hivi. Ndani ya chumba cha kwanza cha haja kubwa kuna mtu amejisaidia bila kusafisha. Pananuka, balaa!

Sehemu ya kusafishia mikono maji yanatiririka. Bomba hazifungi sawasawa. Inaelekea hakuna mtu anayejali kutunza maji. Juu ya sehemu hii ya kusafishia mikono, upande wa kulia, kuna tambara chafu na kuukuu. Sijui nani kaliweka hapa. Labda linatumiwa na wale wanaofanya “usafi” hapa. Sijui ni usafi gani huwa wanafanya. Mahali hapa ni pachafu kupindukia.

Tunapoelekea ndani ya ndege kuelekea Dar Es Salaam, afisa mmoja usalama ananiambia nitoe kofia niliyoivaa. Namuuliza, “Kwanini?” Anasema kuwa hiyo ni kawaida. Abiria lazima watoe kofia ili wasije wakawa wameficha silaha au chochote. Namwambia, “Sidhani kama hii ni kawaida yenu.”

Mwenzake anakuja na kuniambia kuwa kila mtu lazima avue kofia. Namuuliza, “Hata wazungu?” Anajibu, ‘Ndio. Kila mutu” Namwambia kuwa anasema uongo. Mzungu aliyekuwa mbele yangu amevaa kofia ila hakuambiwa aivue!

Nawaambia kuwa nitavua kofia iwapo mzungu aliyepita kabla yangu atarudishwa ili naye avuliwe kofia. “Au wanaobeba silaha na madawa ya kulevya ni ndugu zenu tu?” Nawauliza nikimaanisha Waaafrika. Nagoma kabisa kuvua kofia. Mmoja wa maafisa hawa anamwendea mzungu waliyemwachia apite bila kuvua kofia na kumrudisha ili akaguliwe tena. Nami navua kofia yangu.

Nimetoka ughaibuni ambako watu wenye rangi yetu wanabaguliwa kila kona. Ingawa ubaguzi wenyewe sio wa wazi. Narudi nyumbani nakuta ndugu zangu ndio wanaonibagua! Huzuni inanikaba koo. Afrika yangu itaamka lini?

0 Maoni Yako:

Post a Comment

<< Home

FREE hit counter and Internet traffic statistics from freestats.com