8/16/2004

Mariamu Dukani Kwa Massawe

MARIAMU DUKANI KWA MASSAWE
Kama kawaida yake Mariamu anaomba soda ya bure.
“Soda za bure zimeisha.” Massawe anamjibu huku akijisogeza karibu na dirisha alikojiegemeza. Anaendelea kuomba huku akilegeza macho.
“Soda za bure zimekwisha. Hunisikii?”
“Hizo kwenye friji sio soda? Angekuwa nanihii ungesharuka kumpa duka zima.”

Ni saa mbili mbili asubuhi. Mariamu amejinasua kama kawaida yake. Massawe tamaa kwa Mariamu zimempalia. Lakini leo hataki kutoa soda bure kama afanyavyo kila Mariamu anapokwenda dukani kwake. Amechoka kuwa bwege. Ameanza kuwa “mjanja wa mjini.” Ni miezi sita imepita toka mtoto wa mjomba wake alivyomtoa MOshi na kumleta jijini aje kuuza duka la rejareja lililoko Mbagala Kizuiani.
“Yaani soda nitoe mimi, kufaidi wafaidi wengine.” Anajisemea.

Halafu, “Wewe jana umejifanya kupita kule sio?” Kulikuwa na ahadi ya kukutana jana jioni dukani kwa Massawe kisha waende Mpakani Guest House. Ni mara ya saba hii Mariamu anaacha kutimiza ahadi.
Mariamu anakataa, “Kupita kule wapi?”
“Usijifanye umesahau. Unadhani sikukuona? Ndio bwanako yule?”
“Bwanangu nani?”
“Yule mwendesha mikokoteni hajakupa hela ya kununua soda?”
“Mimi unaona ni mtu wa kununuliwa soda na msukuma mkokoteni?

Massawe anamsogelea Mariamu kama vile anataka kumnusa. Kisha, “Hivi umeoga wewe?”
Leo ni siku ya kumtolea Mariamu uvivu.
“Kwanini nisioge? Labda wewe hapo ndio huogi. Wachagga nyie mnavyopenda hela mnaweza hata mkasahau kuoga.”
“Mbona nasikia harufu ya janaba?”
“Jamani msikieni huyu. Labda wewe ndio unanuka janaba.”
Massawe anaendelea, “Wewe kule ulikolala umeoga?”
“Hebu mwoneni huyu. Kwanini nisioge?”
Massawe anacheka kwa kejeli na hasira iliyojificha, “Yule naye ana bafu? Maji kapata wapi? Bomba lao limekatwa.”
“Wewe ukilala na mwanamke humpi maji?”
“Kama ameyaleta yeye ataoga.”
“He, yaani umchafue tu?!”
“Nani kamchafua nani?”
“Wewe si ndio umemwagia?” Mariamu anasema huku akiondoka. Ameudhika.
“Uchoyo utakuua. Soda moja ya bure ndio imezua yote haya?”
“We unapenda vya bure tu sio?”

Mariamu hajibu. Anaondoka kwa mwendo wa maringo. Massawe anamtazama. Anazidi kumtamani. Donge la hasira na kukata tamaa linamkaba kooni. Kwa miezi miwili amekuwa akitoa soda za bure ila hajafanikiwa. Anashanga: kwanini waendesha mikokoteni, wapiga debe, madereva, makondakta “wanafaidi” ?

Kosa langu nini? Hana jibu. Anaapa kuwa soda za bure hazitoki tena. Kajifunza. Mjini shule, mjini chuo kikuu!

- Mbagala, Dar Es Salaam, Tanzania, 2001

1 Maoni Yako:

At 8/17/2004 05:29:00 AM, Anonymous Anonymous said...

Jamani Masawe! Labda kaepuka ukimwi.

 

Post a Comment

<< Home

FREE hit counter and Internet traffic statistics from freestats.com