8/26/2004

Shairi: UTAWALA BORA LIENDE©

Swali:
Utawala bora liende
Wawala
Nanyi mwalala?

Kura twapiga, sadaka twatoa
Kodi twalipa, swala twasali
Walalanjaa
Cha moto bado twakiona,
Kwanini?

Demokrasia ghasia, mafukara twauziwa
Jehanamu ya moto, masikini twatishiwa
Wa kusema wamesema
Wa kusikia ni viziwi,
Chukua Chako Mapema
Ni azimio la wapi?

Wale wa dini, siasa, enjioo*
Matumbo yamewajaa kwa hadaa
Hawakosi madaha, mzaha
Karaha, zinaa
Unashangaa
Awe yule wa msalaba
Au mwezi na nyota,
Wa bendera ya kijani
Nyeupe au Nyekundu,
Wa ofisi mfukoni
Kutumbulia ufukweni
Dola za wafadhili,
Hao lao moja.

Unafiki wauafiki
Viambaza vya utawala,
Enjioo mtaji poa
Wasomi changamkieni,
Myooshapo kidole kimoja
Vitatu vyawahukumu.

Kanisani, msikitini
Uhaini dhidi ya imani
Isaka, Ismaeli
Mababu wa akina nani?

Nukuu za maandiko
Anguko la kizazi
Dalili zi wazi,
Waza na kuwazua
Kwani kumepambazuka,
Wameasi desturi
Mistari ya manabii,
Kunga za mababu na mabibi
Kwenu tamthiliya ya punguani.

Utamaduni msalabani,
Siasa Babeli Mkuu,
Ijumaa, jumamosi, jumapili
Kwa kanzu na misahafu
Wawarubuni,
Leo katika Bunge
Mchezo wa kuigiza,
Viongozi kuwa "watawala twawala"
Ni aya ipi ya katiba?

Utawala bora liende wawala
Nanyi mwalala,
Ndotoni mkiimba
Amani na utulivu.

Amani na utulivu
Watawala ikulu wadai
Huku wakinywa divai,
Mavazi tai shingoni
Sisi viraka nguoni,
Jasho, kilio, machozi.

Amani, utulivu
Sitaki,
Sihitaji!

- Ndesanjo©, Tanzania/USA (2003)
*enjioo = NGOs (Non-Governmental Organisations)



1 Maoni Yako:

At 8/26/2004 11:04:00 AM, Blogger Ndesanjo Macha said...

Hapo umesema. Sasa ndio umeandika shairi na kumalizia.

 

Post a Comment

<< Home

FREE hit counter and Internet traffic statistics from freestats.com