8/27/2004

VITABU VYA URASTA

Kufuatia mfululizo wa makala nilizotoa katika gazeti la Mwananchi juu ya imani na falsafa ya Urasta, watu wengi wameniuliza wanapoweza kupata vitabu juu ya Urasta. Ukiwa Tanzania, kitabu ambacho kinaweza kupatikana kwa urahisi ni RASTA AND RESISTANCE: From Marcus Garvey To Walter Rodney. Kitabu hiki kiliandikwa na Profesa Horace Campbell wakati akiishi na kufundisha nchini Tanzania na kuchapwa na Tanzania Publishinga House. Nadhani unaweza kukipata katika duka la TPH lililoko mtaa wa Samora, jijini Dar Es Salaam. Kwa walioko ughaibuni, tafuteni kitabu kiitwacho RASTAFARI: Healing of the Nations. Hiki nadhani ni kiboko katika vitabu vyote nilivyosoma juu ya Urasta. Kimeandikwa na Rasta mwanasosholojia, Dennis Forsythe.

Baadhi ya Marasta hawapendi kitabu cha Horace Campbell kutokana na madai kuwa Profesa Campbell ni mfuasi wa itikadi ya Ki-Marx. Marx aliandika kuwa dini ni aina ya ulevi wa kupumbaza masikini ili waweze kutawaliwa. Marx hakuwa akiamini uwepo wa Mungu. Kwahiyo Rasta hao wanaona kuwa mtu kama huyo hawezi kuandika kwa usahihi juu ya imani ya Kirasta.

Campbell mara ya mwisho nilimwona Chuo Kikuu cha Dar Es Salaam. Nadhani ilikuwa ni mwaka 2002 au mwishoni mwa 2001. Yeye kawaida katika mazungumzo yake huwa anatoa heshima kwa Jah Rastafari. Kwa mfano katika hotuba yake pale Mlimani, alimaliza hotuba yake kwa kusema, "Jah!" na waliokuwa wanajua jinsi ya kujibu wakajibu, "Rastafari." Amekuwa kwa miaka mingi akiandika na kutetea imani ya Kirasta katika duru za kitaaluma. Juu ya imani yake sifahamu. Ila nitafanya mawasiliano naye ili kuweka wazi. Kitabu chake nimekisoma na ninaona ni kitabu ambacho kina uchambuzi wa kina na historia ambayo kila Mwafrika anapaswa kuijua. Kuna mambo ambayo sikubaliani naye, ila kwa ujumla naona kitabu hiki kinafaa kusomwa. Hasa zaidi, watu wanaotafuta ukweli juu ya Rasta kwasababu za kitaaluma na utafiti. Kwa masuala ya kiroho, kitabu cha kusoma ni Rastafari: Healing of the Nations.
Jah! Rastafari!

0 Maoni Yako:

Post a Comment

<< Home

FREE hit counter and Internet traffic statistics from freestats.com