8/04/2004

Wakati uliotabiriwa na manabii?

*Naendelea kuwafungulia kitabu cha kumbukumbu. Baadhi ya yaliyomo katika kitabu hiki yametoka kwenye makala yangu ya kila jumapili, Gumzo la Wiki, katika gazeti la Mwananchi. Mengine yatatoka katika kitabu siku za usoni. Haya endelea:
***********************************************************************************

Amsterdam, July 2003:

Aliye mbele yangu ana pasi nyeusi ya Kimarekani. Ni kijana aliyejaza kidogo. Mwamerika Mweusi. Afisa Uhamiaji anaitazama pasi yake kisha anamrudishia. Ni kitendo cha sekunde chache. Pasi yangu ni ya kijani. Anaitazama. Ukurasa wa kwanza, wa pili, tatu, nne… hadi wa mwisho. Anarudi ukurasa wa kwanza. Anaifungua katikati anatazama. Anafungua ukurasa wenye picha yangu, anaitazama, kisha ananitazama kwa muda. Anaitazama tena.

Namkodolea macho. Nataka kumsemesha. Ninaacha. Nina uchovu wa safari. Watu kama hawa ninagombana nao kila siku huku ughaibuni. Nataka kumuuliza kama tatizo ni rangi yangu. Au ni ndevu zangu (ingawa zangu sio ndefu kama za yule bwana anayeishi mapangoni huko Afghanistani!) Au ni nchi niliyotokea?

Tanzania najua ni nchi ya amani na utulivu katika lindi la dhiki, rushwa, unyama wa polisi, na uongo wa kisiasa. Ni nchi ya “uwazi na ukweli.” Au huenda ni kweli vijana wanavyopenda kusema, “Ganda la kijani ni nuksi tupu,” wakimaanisha kuwa pasi ya Kitanzania haina baraka.

Afisa uhamiaji ananiuliza kama nina kadi ya kijani (green card). Nasema ndiyo. Namwonyesha. Anaitazama, anataka kunirudishia, anaitazama tena, kisha ananipa. Niko Amsterdam njiani kuelekea Tanzania. Hali ya dunia imebadilika. Vita. Hofu. Ugaidi. Uvumi wa vita. Mabomu ya kujitoa mhanga. Na bila kusahau silaha za maangamizi!

Nakumbuka wimbo wa Bob Marley wa Real Situation. Anasema:

Check out the real situation Nation war against nation.Where did it all begin?When will it end?Well, it seems like: total destruction the only solution,And there ain't no use: no one can stop them now.Ain't no use: nobody can stop them now

Maneno haya yanaelezea wakati tunaoishi leo hii. Labda huu ndio ule wakati ulionenwa na “manabii wa kuja.”

0 Maoni Yako:

Post a Comment

<< Home

FREE hit counter and Internet traffic statistics from freestats.com