10/13/2004

JINSI YA KUONDOA SERIKALI MADARAKANI

Nimekuwa nikiandika makala hii kwa muda mrefu. Ni makala inayoonyesha jinsi ambavyo watu wa kawaida wanaweza kuondoa watawala madarakani na kuweka viongozi/kujiongoza wenyewe. Nadhani nitaimalizia leo usiku na kuituma katika safu yangu ya gazeti la Mwananchi. Kabla ya mwisho wa wiki ijayo nitaiweka hapa ndani ya blogu. Nimemaliza kusoma kitabu kiitwacho: JINSI YA KUWATOA WANAUME WAZUNGU MAJUHA MADARAKANI. Kitabu hiki kimenitia moyo wa kumalizia makala yangu. Kitabu bomba sana hiki. Kwa walio Tanzania, fuatilia Mwananchi na walioko nje ya Tanzania, fuatilia blogu hii ili uweze kusoma makala hiyo. Nadhani ni jambo muhimu sana kujua jinsi ambavyo sisi watu wa kawaida tunaweza kuwaondoa madarakani watawala ambao wamezungukwa na kuta nene na polisi wa kuzuia fujo na jeshi ni kama misukule yao. Kama unamsikiliza Fela Kuti, kasikilize wimbo wake wa Zombie (Msukule). Alipoimba wimbo huu nchini Ghana, ilibidi serikali imtumie haraka sana. Wimbo huu unazungumzia askari kama tunaokumbana nao barabarani tunapoandamana. Utakuta tunatetea haki ambazo zinawajumuisha ndugu zao, wao wenyewe, majirani zao, shangazi zao, bibi zao, watoto wao, nchi yao, n.k. lakini kwakuwa eti wamepewa "amri" wanakurupuka na kuanza kutuangushia mkong'oto. Usikose makala hiyo. Lazima tujiongoze wenyewe. Nguvu za demokrasia ziwe mikononi mwetu. Kuna kanuni za umma kutwaa madaraka. Kwa maneno mengine nitakuwa nazungumzia jinsi ya kuleta mapinduzi. Najua CCM wanaamini kuwa wao ndio wana haki ya kuzungumzia mapinduzi. Wengine tukizungumzia tunaweza kukamatwa na kushtakiwa kwa uhaini. Sijui kwanini wanaongopa watu wa kawaida tukitumia neno hili. Tuna haki ya kusema kuwa tunataka mapinduzi. Kwani tunachotaka sio kitu kingine. Harambee!
"By Any Means Necessary." - Malcolm X.

0 Maoni Yako:

Post a Comment

<< Home

FREE hit counter and Internet traffic statistics from freestats.com