10/10/2004

MAZINGIRA NA HATIMA YA TANZANIA

Kwa wale wanaopenda kufuatilia masuala mbalimbali ya mazingira nchini Tanzania (sheria, sera, uharibifu, uzembe, utafiti, n.k.) nenda katika webu ya jamaa wa LEAT: http://www.leat.or.tz/. Hawa mabwana wanafanya kazi nzuri sana. Nenda katika webu yao kajielimishe juu ya masuala ya mazingira nchini Tanzania. Jambo moja ambalo nadhani tunapaswa kuwauliza ni hili: hizi taarifa kwenye webu yao ni kwa ajili ya nani? Kama ni kwa ajili ya Watanzania, kwanini waandike kwa lugha ya watu wengine? Watanzania, ambao ndio wanapaswa kujua undani wa masuala ya mazingira yao, kupata taarifa sahihi ili waweze kushiriki katika harakati za utunzaji wa mazingira; lugha wanayoielewa ni Kiswahili. Wiki kadhaa zilizopita niliandika makala ambayo nitaiweka bloguni hivi karibuni ambayo kimsingi ilikuwa ikihoji mantiki ya waanzishaji wa vyama vya siasa au mashirika yasiyo ya kiserikali yenye majina ya Kiingereza. Tazama chama kama NCCR-Mageuzi, kwa mfano, sijui ni wakulima na wafanyakazi wangapi ambao chama hiki kinadai kuwatetea wanaoweza kusema kirefu cha NCCR. Nakumbuka kuna wakati chama hiki kilikuwa na mwenyekiti ambaye hakuwa anaweza kutamka vyema kirefu cha jina hili. Je ni wakulima na masikini wangapi wanaelewa maana ya maneno Tanzania Labour Party au Civic United Front. Ukiona majina ya mashirika yasiyo ya kiserikali na vyama vya siasa unaweza kufikiri kuwa uko Uingereza au Australia. Huwezi kuanzisha chama au shirika kwa ajili ya Watanzania kisha ukakipa au ukalipa jina la kigeni ambalo Watanzania hao unaotaka kuwatetea au kuwaelimisha hawawezi kutamka wala kuelewa maana ya jina la chama au shirika lenyewe. Kuna sababu kuu mbili zinafanya jambo hili kutokea. Kwanza, kasumba ya kuamini kuwa jina la Kiingereza lina utamu zaidi maana hii ni lugha yenye hadhi zaidi duniani. Kiongozi yeyote mwenye fikra kama hizi anahitaji msaada wetu. Anahitaji kuongozwa na sio kuongoza. Sababu ya pili ni kuwa mashirika na vyama vinaanzishwa kwa ajili ya wafadhili. Kwahiyo majina yanachaguliwa toka kwenye lugha ambayo wafadhili wanaielewa. Ujumbe mkuu wa blogu hii ni kujikomboa. Lazima tupambane vikali na upuuzi huu. Mtu yeyote anayekuja kuomba kura kwako na chama ambacho jina lake linatumia lugha ya Kiingereza mwambie aende akashiriki uchaguzi wa Uingereza au Canada. Watanzania lugha yetu ni kiswahili. Hii ndio lugha ya walalanjaa. Ndio lugha ya wakulima na wafanyakazi wanaonyanyaswa na mfumo wa utawala wa watu wachache wenye fedha na elimu. Wenye fedha wanatumia uwezo wao kuturubuni na kuweka viongozi kwenye viganja vyao na wenye elimu wanatumia elimu yao na lugha ya kuja kutuweka kizani na kuendeleza ukoloni mamboleo huku wakishirikiana na watu wanaoitwa wafadhili. Upuuzi huu, utumwa huu wa kiakili ukome.

Kwahiyo ndugu yangu tembelea webu ya jamaa wa LEAT. Nakuomba utumie dakika chache kuwandikia na kuwataka waonyeshe heshima sio kwa mazingira tu bali pia kwa utamaduni wetu na lugha yetu. Waulize kama webu yao ni kwa ajili ya wafadhili na wazungu tujue. Ila kama taarifa zilizoko hapo ni kwa ajili ya kuwawezesha Watanzania, basi watumie lugha ambayo wote tunaielewa vyema. Anuani yao hii hapa: leat@mediapost.co.tz . Ukiweza tuma kopi hapa: ughaibuni@yahoo.com
Unaweza pia ukawatumia kipande hiki kwa kubonyeza hapo chini kwenye alama ya kibahasha kisha uweke anuani yao hiyo hapo juu. Au unaweza kuwaandikia barua wenyewe. Taarifa zilizoko kwenye webu yao ni za muhimu mno ndio maana ninaona ni muhimu kwa lugha ya Kiswahili kutumika. Taarifa hizi zitakuwa na mafanikio zaidi zikitufikia kwa lugha tunayoijua. Lugha tunayoitumia asubuhi, mchana, na jioni. Hata hivyo, nawapongeza jamaa wa LEAT kwa kazi kubwa wanayoifanya. Kwakuwa masuala ya mazingira hayako kwenye kauli za wana si-hasa wetu ni vyema kukawa na makundi ya wana wa nchi kama LEAT yanayohamasisha na kutetea utunzaji wa dunia tuliyorithishwa na waliotutangulia ambao waliitunza na kuiheshimu... na hata kuiabudu!

0 Maoni Yako:

Post a Comment

<< Home

FREE hit counter and Internet traffic statistics from freestats.com