12/11/2004

YESU! KIIRU! BLOGU LAKI MBILI ZA WAIRANI!

Irani ni moja ya nchi ambazo teknolojia ya blogu imevaliwa njuga na wananchi wake. Hii ni nchi ambayo uhuru wa fikra, habari, na mawasiliano unawekewa vizingiti na utawala wa wanaojiita waislamu. Hivi karibuni niliandika juu ya wanablogu waliokamatwa kwa kutoa mawazo yao. Kuna zaidi ya blogu 200,000 (laki mbili) za Wairani. Kati ya hizo, 65,000 zinaandikwa kwa lugha inayozungumzwa na wengi nchini humo, Parsi. Lugha hii ndio ya nne kwa umaarufu katika ulimwengu wa blogu. Pamoja na kukamatwa kwa wanablogu wa nchi hiyo, blogu imebaki kuwa ndio chombo cha habari ambacho watawala wa nchi hiyo wameshindwa kukikaba koo kama vyombo vingine kama magazeti kama makala hii inavyotupasha. Wakati wenzetu Irani wana blogu laki mbili, Tanzania tuna blogu tatu. Na katika hizo, wanablogu wa Furahia Maisha Yako na Kona Yangu sijui nini kimewatokea. Wamekuwa kimya. Huyu wa Kona Yangu alikuwa anaandika juu ya mambo ya "wakubwa." Isije ikawa kaambiwa afunge domo lake kubwa! Unajua wa-twawala wasivyopenda kuambiwa ukweli. Kama wanavyotudanganya ili tuwape kula, nao wanataka tusiwape ukweli wa mambo. Wanataka tuwe waongo kama wao. Wanataka tufanye kati ya haya: 1. Funga domo! 2. Kama ukishindwa, ukiufungua usiseme ukweli hata kama hizi ni "zama za ukweli na uwazi." Kuna wakati niliuliza kama midomo hiyo wanayotumia kudanganya umma wanawezaje kuitumia makanisani na misikitini?

0 Maoni Yako:

Post a Comment

<< Home

FREE hit counter and Internet traffic statistics from freestats.com