1/10/2005

USIMSAHAU MARTIN LUTHER KING, JR

Mwaka 1988, Rais Reagan (Reagan?!!, unaweza usiamini) alipitisha sheria ya kufanya kila jumatatu ya tatu ya mwezi Januari kuwa ni siku ya kukumbuka maisha, harakati, na falsafa za Dr. Martin Luther King, JR. Hii ndio sikukuu pekee inayoazimishwa kwa ajili ya mtu mweusi hapa ndani ya tumbo la Jitu (Nadhani unafahamu kwanini Malcolm X hana sikukuu ya kitaifa.)
Kwahiyo jumatatu ijayo ni sikukuu ya Dr. King. Ingawa sikukuu hii ya Dr. King ni ya kitaifa kuna majimbo ambayo hayaisherehekei. Kuna watu wengi ambao wanapinga kuwepo kwa sikukuu hii. Pia kuna waliotaka sikukuu iwe siku aliyozaliwa. Wengine wakataka siku aliyouawa. Hata kupitishwa kwake na bunge kulikuwa kwa kushikana mashati. Siku nne baada ya kuuawa kwa Dr. King mwaka 1968, mbunge wa chama cha Democratic wa Michigan, John Conyers, alipeleka muswada bungeni wa kutaka kuwe na sikukuu ya Dr. King. Ilichukua miaka 20 kwa sheria ya kuwa na sikukuu hii kupitishwa!
Kauli mbiu ya sikukuu hii kila mwaka ni hii: "Remember! Celebrate! Act! Day On, Not A Day Off!!"
Historia ya Dr. King ni ndefu. Moja ya mambo aliyofanya King ni kuongoza moja ya mgomo uliochukua muda mrefu katika historia ya migomo Marikani na duniani. Aliongoza mgomo wa mabasi kupinga sheria ya kubagua abiria kutokana na rangi zao. Mgomo huu ulidumu kwa siku 382 hadi pale Mahakama Kuu ya Alabama ilitamka kuwa sheria hiyo ilikuwa inakiuka katiba ya nchi.
Mwaka 1963 aliongoza moja ya moja ya maandamano makubwa katika historia ya Marekani yaliyoitwa "March on Washington." Ni katika maandamano haya ndipo alipotoa hotuba yake maarufu ya "Nina Ndoto" (I have a Dream).
Mwaka 1964 Dr. King alitunukiwa nishani ya amani ya Nobeli. Wakati wa kupokea tuzo hiyo alisema haya. Hotuba yake ya Nobeli nayo ina ujumbe mzito kuhusu mwanadamu na masahibu yake.
Dola 54,000 za Kimarekani alizopata kutokana na tuzo hii alizitumia kununulia vihamba (mashamba), magari ya kutanulia na kusafishia jina, na kujenga majumba ya kifahari ufukweni mwa bahari,!...We! Nakutania. Aligawanya fedha hizo kwa vyama vilivyokuwa vikipigania haki na usawa. Unadhani Dr. King alikuwa kama viongozi wetu fulani na fulani ambao majina yao unayajua?
Mwaka 1968 Dr. King aliuawa kwa risasi kama ilivyotokea kwa Malcolm X mwaka 1965. Au Mahatma Gandhi kule India. Au Lumumba. Au Che Guevara.
Sasa katika kumkumbuka Dr. King nakuomba usome aliyoandika (hasa katikati na mwishoni) kwenye Barua Toka Gereza la Birmingham. Pia ukienda hapa utaona aliyosema kuhusu vita na amani na pia hotuba zake zinazopendwa na wengi.
Muhimu zaidi msikilize kwa sauti yake mwenyewe akitoa hotuba yake ya "Nina Ndoto." Kongoli hapa.

0 Maoni Yako:

Post a Comment

<< Home

FREE hit counter and Internet traffic statistics from freestats.com