7/06/2005

Nimetia mguu Gleneagles waliko makuhani wa ubepari

Tumerudi nyumbani toka Gleneagles, mwendo wa kama saa moja na nusu. Mpango uliopo hapa ni kuwa basi linaondoka toka hoteli ya Hilton? Sheraton? (sikumbuki...zote zinafanana) kupeleka waandishi wa habari. Basi tumefika pale tukashuka kwenye gari kisha tukapita sehemu ya kusachiwa, "Weka begi hapa, toa vitu mfukoni, njoo hapa, nyanyua mikono juu, onyesha soli ya viatu vyako..." Hizi ndio amri unazokutana nazo. Lakini kwa ujumla askari ambao nimekutana nao hapa toka nije ni wastaarabu sana. Baada ya kusachiwa tuliingia kwenye basi jingine dogo ambalo lilitupeleka kwenye kituo cha waandishi wa habari. Pale tukakabidhiwa begi. Kila mwandishi anapewa begi hili ambalo ndani yake lina biskuti, chokoleti, magazeti, na wiski aina ya Black Label ambayo imevundikwa kwa miaka 12. Wakati wanatupa nilitaniwa wenzangu, "Wanatuhonga nini?"
Ukiona kiasi cha fedha zilizotumika kwa mkutano huu ambao makuhani wakuu wa ubepari wanakutana kwa masaa sijui mawili kwa siku huwezi kuamini. Kwanza nilipokuwa ndani ya basi baada ya kulala, kuamka, kulala, na kuamka tena, nilijiuliza: Kwanini viongozi waliochaguliwa na watu waje kujificha mbali hivi? Eneo lote limezungushwa waya, juu kuna helikopta zinazunguka, chini askari wamejaa kila upande...kweli hawa ndio makuhani wakuu.
Basi tukaenda kwenye tafrija ya waandishi wa habari ambapo kulikuwa na maakuli ya nguvu ya Kiskoti, mvinyo, wiski, na vitu vingine ambavyo majina yake sijui na sikuthubutu kuuliza nisionekane kuwa nimeshuka mjini leo! Hivi majuzi Rais wa Ufaransa, Chirac, alidai kuwa mapishi ya Uskoti ndio mabaya zaidi Ulaya baada ya mapishi ya Ufini. Waingereza wamechukia na kudai kuwa, "afadhali yetu sisi hatuli konokono na miguu ya chura." Jamaa ambaye anatuandalia chai asubuhi ni Mfaransa, leo nilimuuliza kama amewahi kula miguu ya chura akacheka karibu akaukie.
Wakati tunajichana tuliambiwa mambo kadhaa kuhusu nchi ya Uskoto: simu, luninga, dawa ya penisilini, vyote viligunduliwa hapa. Mfumo wa kileo wa vyuo vikuu na vitivo ulianzia hapa. Uskoti inaongoza kwa utoaji wa machapisho ya kitaaluma duniani (ukilinganisha machapisho na idadi ya wananchi wake).
Wakati tunajichana tulipitiwa na mkutano wa waandishi wa habari na Bono na kampuni yake. Maura, mwandishi tuliye naye hapa toka Msumbiji, amesikitika sana kutomuona Bono. Anapenda sana miziki ya kundi la Bono la U2. Msome Maura akizungumzia muziki wa rapu kule Msumbiji.
Mapema leo kulikuwa na mapambano kati ya polisi na waandamanaji. Kulikuwa pia na maandamano yaliyopewa kibali yaliyoongozwa na akina Bono na Geldof. Imeshangaza wengi kuona kuwa serikali ya Uingereza inavyounga mkono akina Bono na pia waandaaji wa Make Poverty History. Unaweza kuamini kuwa waziri wa mambo ya misaada ya kimataifa wa Uingereza, Hilary Ben, alikuwa kwenye maandamano ambayo wengi waliamini kuwa yalikuwa yakipinga ubepari. Maandamano ya kuipinga serikali yanahudhuriwa na mtumishi wa hiyo serikali. Watu sasa wameanza kusema kuwa hawa wakuu wa makuhani wametuzidi kete maana hata maandamano wanaandaa wao kwa kutumia watu wengine.
Jioni saa kumi nilikuwa kwenye mjadala unaohusu uwezo wa maandamano kubadili jamii kwenye kipindi cha Simon Mayo Radio Five Live. Muda sio mrefu uliopita, Joel, ambaye amewasili leo toka Uganda alifanya mahojiano na radio open source. Mahojiano hayo hayakumalizika maana mawasiliano yalikatika.

Sasa nitaandika kifupi juu ya siku ya kwanza kufika pale Gleaneagles kwa ajili ya blogu ya Panos, kisha nikalale maana kesho asubuhi na mapema tunakwenda kule waliko wezi wakuu wahedi! Ratiba inaonyesha kuwa msafara wa rais wa Tanzania utawasili kesho. Nimepewa namba ya kupiga ili kujua kama Mkapa atapatikana kwa ajili ya mahojiano.

1 Maoni Yako:

At 7/07/2005 01:34:00 AM, Blogger Indya Nkya said...

Bono na Geldof, Blair na Kichaka lao moja. Huo ni uiigizaji tuu.

 

Post a Comment

<< Home

FREE hit counter and Internet traffic statistics from freestats.com