7/02/2005

Polisi Edinburgh

Pamoja na ukweli kuwa polisi walikuwa wamejaa kila kona wakati wa maandamano, polisi hawa hawakuwa kama askari wa Tanzania ambao wana kazi kubwa mbili: kunyanyasa wananchi au kula rushwa. Niliwaendea polisi mara tatu kutaka msaada: kuuliza njia, kutafuta choo, na mgahawa. Askari waliongea nami kwa upole kama vile mimi ni ndugu yao. Amani iliyotawala maandamano hayo ilitokana na sababu nyingi, mojawapo ni kitendo cha polisi kuwa walinzi kuhakikisha watu wanaandamana vyema. Nchi nyingi Afrika (hata nchi za Magharibi) ukiwa uaandamana, ukiona polisi unajua kuwa utaona cha mtema kuni siku hiyo.

Katika mambo yaliyoniingia sana wakati wa maandamano ni vikundi vya ngoma. Sikuona kundi hata moja linalopiga ngoma kama wanajifunza. Makundi yote yalikuwa kama vile yako mashindanoni. Acha tu, hadi hivi sasa nasikia milio ya ngoma kichwani. Ngoma zilikung'utwa sio mchezo. Kingine kilichoambatana na ngoma ni filimbi.

Hivi sasa Stevie Wonder yuko jukwaani katika tamasha la Live 8.

Baada ya kutumia muda mwingi kuhojiana na waafrika waliokuwa wakiandamana, nilikwenda kwenye mgahawa mmoja kujipatia kitu cha kuingiza mdomoni maana nilikuwa karibu nianguke kwa njaa. Utamu wa kuwa katikati ya ngoma, nyimbo, dansi, filimbi, mabango, kelele, n.k. ulinifanya sikujua kuwa karibu "nife" njaa. Wakati natoka kwenye mgahawa nilishtuka kuona watu wote wanaoandamana wamesimama na kukaa kimya. dakika chache zilizopita mtaa mzima ulikuwa umejaa kelele, lakini sasa ghafla kimya. Kulikoni? Mara wakati najiuliza watu wote wakapiga mayowe, makofi, na mbinja kwa ghafla. Baadaye nakuja kujua kuwa ilipofika saa tisa kamili kila mtu alitakiwa kukaa kimya kwa dakika moja.
Nilikutana na jamaa wa kundi la Revolution, ambalo ni tawi la vijana la chama cha Socialist Workers Party. Wakati maandamano yalikuwa na ujumbe kuwa Make Poverty History (Fanya Umasikini Uwe Historia), wao walikuwa wakisema: Make Capitalism History. Niliongea nao kwa muda. Waliniambia kuwa mpango mzima wa Make Poverty History haufai maana nia yake ni kushawishi viongozi wa nchi za kibepari walete mabadiliko wakati ambapo dawa ya umasikini kuuondoa kabisa mfumo wa kibepari. Wanasema kuwa ubepari unahitaji umasikini kwahiyo huwezi kutumia mfumo wa ubepari kuondoa umasikini wakati ambao msingi wa mfumo huo ni kuwepo kwa tabaka la wanaonyonya na wanaonyonywa.

Kwahiyo suluhisho ni nini? Niliwauliza. Jibu lao ni kuwa serikali za kibepari zinapaswa kupinduliwa na mfumo mzima wa uchumu kujengwa upya. Hakuna kupoteza muda kujadiliana na manepari, waondoe madarakani kwa njia yoyote ile.

Kwa taarifa yako: gharama ya ulinzi wa washiriki wa mkutano wa G8 na eneo lenyewe ni kubwa zaidi ya pato la mwaka la nchi kama Malawi!

Tazama picha hapa za maandamano.

1 Maoni Yako:

At 7/03/2005 11:45:00 AM, Anonymous Anonymous said...

Huko
kwenye 8
mambo yakoje? wanaongelea unafuu wakuwalipa au kutulipa? itamsaidiaje
mawazo
wa tandale kupat njia nzuri ili akiugua awahi na kupata matibabu pale
mwananyamala hospitali? sijui nini tunangojea. wanaita live8 wanalengo
wanalosema au kwa wengi ni sehemu ya kupata wavuta madawa ya kulevya
wenzao
na ngono za hadharani.

 

Post a Comment

<< Home

FREE hit counter and Internet traffic statistics from freestats.com