7/05/2005

Wakulima wa Uskoti, eco-village, n.k.

Leo waandishi wote toka Afrika na wafanyakazi wa Panos London tuna furaha maana tumepata vitambulisho vya kutuwezesha kuingia unakofanyika mkutano wa wezi wakuu duniani. Kwa maana hiyo huenda nikagongana na Joji Kichaka akiwa ametoka chooni. Sijui nitamwambia nini. Nadhani nitabadili njia. Kipenzi chao mkuu, rais wa Tanzania, Benjamin Mkapa (au Makapa kama jinsi wazungu wanavyotamka) naye atakuwepo. Naye nikukutana naye sijui nimwambie nini. Najua cha kumwambia. Nitamkaripia (ndio, rais ni mtumishi wetu) kisha nitamwamuru arudi Tanzania haraka sana aachane na hawa wezi watamlostisha!
Asubuhi leo tumekutana na viongozi wa chama cha wakulima wa Uskoti, NFU-Scotland. Mazungumzo yetu nao yalihusu ruzuku kwa wakulima wa Ulaya na Marekani na masahibu ya wakulima wa Afrika. Hawa jamaa wanasema kuwa ni kosa kubwa sana kwa wanaharakati kudai kuwa nchi za Ulaya ziache kutoa ruzuku kwa wakulima wake. Wanasema kuwa watu wengi hudhani kuwa wakulima wote Ulaya ni matajiri wakati ambapo wanachama wao wengi wana mashamba ya kawaida tu tofauti na wakulima kama wa Marekani. Wakatuambia kuwa kuna hatari ya kuwafanya wakulima duniani waanze kugombana wao kwa wao wakati ambao wana maslahi yanayofanana.
"Sisi hatuna sababu ya kugombana na wakulima wa Afrika. Ila vyombo vya habari vikiandika kuhusu wakulima vinatoa picha ambayo inaweza kuleta hali ya kuchukiana. Sisi sote ni wakulima." Mkurugenzi wa chama hicho, Andy Robertson alituambia.
Kwa maana hiyo, wakati baadhi ya wanaharakati wanadai kuwa nchi za Ulaya zisitoe ruzuku, wakulima hapa Uskoti wanasema kuwa ruzuku itolewa kwa wakulima dunia nzima. Ila wanataka ruzuku inayotolewa isiwe ni ile inayoharibu bei za bidhaa za mashambani kwenye soko la dunia.
Tulipowauliza kuwa hawaoni kuwa kitendo cha serikali yao kuwapa ruzuku kinawapa uwezo zaidi wa kushindana na wakulima wa Afrika ambao wana uwezo kidogo, walidai kuwa kwa kiasi kikubwa washindani wao sio wakulima wa Afrika. Sababu ni kuwa wao hawalimi pamba, kahawa, chai, tumbaku, n.k. Wanasema mazao wanayolima sio mazao ya wakulima wa Afrika. Kwa ufupi, wakulima wa Uskoti wanachukia sana wanaposikia wanaharakati wakitaka serikali ya nchi hii kuacha kutoa ruzuku.
Mchana wa leo tulikwenda kwenye kijiji kiitwacho Eco-Village. Ni umbali kama wa saa moja hivi toka hapa. Kijiji hicho ambacho ni cha muda kiko chini ya watu wanaotaka kujenga jamii zenye kujali mazingira na demokrasia ya moja kwa moja. Tulipofika hapo tulikutana na mtangazaji wa BBC ambaye pia ni mwanablogu, Paul Mason, akatuambia kuwa waandishi hawaruhusiwi kuingia ndani ya kambi. Tunachoweza kufanya, alituambia, ni kuongea na wahusika nje ya kambi hiyo. Basi tukaamua kuuza maneno. Nilikuwa mimi, Machrine toka Uganda na Dr. Banda wa Panos Kusini mwa Afrika. Tukasema tumetoka Afrika, sisi sio sawa na waandishi wa magazeti makubwa hapa Uingereza. Nikaingiza hii: nimetoka Tanzania ambapo tulikuwa tuna siasa ya ujamaa inayofanana na itikadi ya kijiji chao.
Wakadai wamekubaliana kuwa hakuna waandishi maana waaandishi huwa wanawaandika vibaya. Basi mmoja wetu akauliza, "Unaweza kutuitia kiongozi tuongee naye? Nani mwenye kauli ya mwisho?" Swali hili tuliuliza maana hatukuwa tukijua kwa undani itikadi yao. Basi dada aliyekuwa akiongea nasi akashtuka na kusema, "Hapa hatuna mtu anayeitwa kiongozi, hatuna madaraja au matabaka. Hatuna mtu mmoja anayeamua kwa ajili ya wengine. Ndio maana tunapinga mfumo wa demokrasia ya uwakilishi. Maamuzi yetu tunafanya kwa makubaliano."
Baada ya "kuwalilia" sana waliamua kujadiliana na baada ya muda wakatuambia tumeruhusiwa kuinga kijijini ila lazima tuache rekoda, kamera, kalamu, kila kitu nje ya kijiji. Basi hapo tukaingia ndani. Ndani kuna nini? Rudi tena nitaendelea kwani nina kazi ya kumaliza kabla ya kulala na kesho asubuhi kwenye Gleaneagles kunakifanyika mkutano wa "kuigawa" Afrika kama alivyofanya Bismarck. Kazi ninayofanya ni kuandika habari kuhusu kampuni ya City Water iliyokuwa imepewa jukumu la kubinafisha maji jijini Dasalama. Toka tufike hapa nimekuwa nikifuatilia suala hili ikiwa ni pamoja na kuonga na Cliff Stone, mmoja wa wakurugenzio waliofukuzwa nchini.
Tafadhali tazama wanablogu wa Afrika wanasema nini juu ya tamasha la muziki la wazungu la "kutetea" Afrika la Live 8. Msome John Kamau akiblogu kwenye BBC Online. Nisome kwenye gazeti la Metro la hapa kwa Blair. Kisha fuatilia mjadala huu hapo kesho.

0 Maoni Yako:

Post a Comment

<< Home

FREE hit counter and Internet traffic statistics from freestats.com