8/02/2005

Nguvu Mpya, Mtazamo Ule Ule

Haya nimerudi. Nguvu mpya, mtazamo ule ule. Katika kipindi hiki cha ukimya nimefanya mambo kadhaa. Kati ya niliyofanya nimesoma kitabu kitwacho You Are Being Lied To : The Disinformation Guide to Media Distortion, Historical Whitewashes, and Cultural Myths. Kitabu hiki ni mkusanyiko wa makala za watu mbalimbali zilizohaririwa na Russ Kick wa kampuni ya Disinformation. Kuna makala moja iliyoandikwa na David Thomas, The Bible Code: Scientific, Statistical Proof of God? Or Just Another Lie? Makala hii inatokana na kitabu kilichopigiwa makofi sana na wakristo wenye msimamo mkali kiitwacho The Bible Code. Kitabu hiki kilichotolewa mwaka 1997 na mwandishi wa habari Michael Drosnin kinadai kuwa ndani ya Biblia kuna ujumbe wa siri. Unaweza kujua ujumbe huu kwa kuunganisha herufi na namba kadha wa kadha. Mwandishi David Thomas kwenye kitabu cha You are Being Lied To anasema kuwa kwa kutumia kanuni iliyotumiwa kudai kuwa Biblia ina ujumbe wa siri unaotabiri dunia ya kesho hatakuwa amekosea akisema kuwa hata vitabu kama War and Peace cha Tolstoy, Origin of Species, na Kurani vina ujumbe wa siri kwa wanadamu. Kwa kutumia kanuni za mahesabu alizotumia Drosnin kuandika kitabu chake cha The Bible Code utapata ujumbe kama alioupata kwenye biblia kwenye vitabu hivi. Sio vitabu hivyo tu vina “bible code” bali pia aliweza kupata ujumbe wa siri kwenye maoni ya mhariri ya gazeti la the Chicago Tribune na Unabomber Manifesto ya Ted Kaczynski. Soma hapa kwa habari zaidi kuhusu dhana ya "bible code."

Lakini sehemu niliyoisoma na kushukuru mababu kuwa mbavu zangu ziko salama ni mahojiano kati ya Russ Kick na “Baba Mtakatifu” wa watu wasioamini kuwa kuna mungu, Warren Allen Smith. Mahojiano haya yalihusu kitabu alichoandika Warren Smith kiitwacho Who is Who in Hell. Smith anaonyesha jinsi dunia yetu ilivyojaa vitu kama vitabu, majengo, teknolojia, picha, vituo vya luninga, muziki, n.k. vilivyotokana na kazi za watu wasiomwamini mungu. Anasema kuwa kama unaamini kuwa watu wasiomwamini mungu ni makafiri na mashetani basi usitumie Intaneti, Hotmail, Microsoft Word, Internet Explorer maana vyote hivi vimetokana na “makafiri” wasiomwamini mungu. Pia usitazame CNN au sinema kama The Godfather, Jurassic Park, Chinatown, usiingie katika majengo yaliyobuniwa na mbunifu maarufu wa majengo duniani Frank Wright, usitazame michoro ya Picasso, Frida Kahlo, usisikilize miziki ya R.E.M, Mozart, Beatles, Beethoven, Barry Manilow, n.k., usitumie “pasteurized milk” (maziwa ya mtindi ya kwenye makopo), usitumie huduma za shirika la Msalaba Mwekundu, usisome vitabu kama The Great Gatsby, Robinson Crusoe, Oliver Twist, A Tale of Two Cities, Moby Dick, The Three Musketeers, The Grapes of Wrath, The Color Purple…kazi/vitu vyote hivi vimetokana/milikiwa na watu wasio na dini au kuamini mungu.

Nimekuwa pia nikisikiliza CD ya Fight to Win ya Femi Kuti. Wimbo uitwao ’97 umenihuzunisha kiasi maana anaimba juu ya kifo cha baba yake, Fela, na dada yake ‘Sola. Anakumbuka jinsi maelfu ya watu walivyotembea kwa masaa saba (kutokana na kujaa watu) kwenda kupumzisha roho wa Fela katika nyumba ya Eledumare. Katika wimbo mwingine anasema kuwa watawala wa Afrika ambao wanaiharibu na kuua watu huku wakiwatumikia wazungu lazima tuwatambue kwa jina lao halisi: Wasaliti wa Afrika.

Na wasaliti wa Afrika ndio nitakuwa nawazungumzia sana. Hasa nitakapokuwa nikiandika kuhusu ule mchezo wa kuigiza niliohudhuria kule Uskoti na maendelezo ya mchezo huo. Pia tutakavyokuwa tukikaribia Wizi Mkuu Tanzania hapo Oktoba tutakapotakiwa kuchagua “mwizi huyu au yule.”

Na hivi jamani
John Garang, helikopta ile ilianguka kwa matatizo ya hali ya hewa au ilitunguliwa?
Haya. Nina barua pepe elfu kumi kidogo za kusoma na kujibu. Makala za kuandika na nyingine mpya za kupandisha. Pia makala mpya za padri Karugendo. Na mapitio ya blogu za Kiswahili kwa ajili ya Global Voices. Bila kusahau makala na vipande toka mchezo wa kuigiza wa wakuu wa makuhani wa ubepari, yaani G8, na uzoefu wa kublogu wa waandishi wengine toka Afrika kupitia Panos.

2 Maoni Yako:

At 8/03/2005 03:41:00 AM, Blogger Indya Nkya said...

Karibu tena. Umekuja na nguvu mpya tunasubiri mengi sana. La Garang bado linasikitisha mno.

 
At 8/04/2005 09:01:00 AM, Anonymous Anonymous said...

Hata mimi naunga idya nyka mkono akisema 'karibu tena', ndesanjo.

Nimecheka sana kusoma maoni ya Warren Allen Smith:)

 

Post a Comment

<< Home

FREE hit counter and Internet traffic statistics from freestats.com