8/04/2005

Nilikuwa nasema nini tena?

Wiki hii ndio kumbukumbu ya unyama wa Marekani dhidi ya wakazi wa Hiroshima na Nagasaki. Hapo mwaka 1945 Marekani ilikuwa taifa la kwanza na pekee kutumia silaha za maangamizi dhidi ya raia wasio na hatia yoyote dhidi ya nchi hii. Mabomu ya atomiki yaliangushwa na kuua wengi na mionzi ya sumu kuathiri hata wale ambao walikuja kuzaliwa baadaye.

Nimesikia mahojiano, ingawa dakika za mwisho, katika redio ya
NPR, ya mmoja wa marubani waliorusha madege yaliyoangusha mabomu hayo. Bwana huyo anasema kuwa hajuti hata kidogo na wala hakosi usingizi. Anasema kuwa anaamini kabisa kuwa uamuzi wa kuangusha mabomu hayo ulikuwa ni sahihi kwani baada ya unyama huo vita wanavyoita vya dunia visingemalizika.

Historia hii ya matumizi ya silaha za maangamizi huko Japani ni muhimu sana katika kipindi hiki ambacho Marekani inaambia nchi kadhaa duniani kuwa hazina haki ya kuwa na silaha za nyuklia, sumu, na baiolojia. Wakati Marekani ndio nchi pekee ambayo imetumia silaha hizo dhidi ya nchi nyingine na ndio nchi yenye silaha nyingi na hatari kabisa kuliko nchi yoyote duniani, imesimama kidete kama vile haina mshipa wa aibu kutaka nchi kama Korea ya Kaskazini na Iran zisiwe na silaha hizo.

Unaona uchaguzi wa Irani hivi majuzi.
Rais mpya wa Irani amechaguliwa kwasababu ya Marekani. Marekani haimpendi lakini ajabu ni kuwa Marekani hiyo ndio ilimpa Urais. Wairani hawataki nchi nyingine eti ijipe haki ya kuiambia nchi yao ifanye nini na nini isifanye. Hivyo wako waliopiga kura kuchagua mtu ambaye ambaye siasa zake ni za kuiambia Marekani, “Nendeni kuzimu.”

Nani kaipa Marekani hiyo haki ya kuamua nchi zipi zina haki ya kuwa na silaha kali kama za nyuklia? Kwanini Marekani iwe na haki ya kuwa na silaha hizo lakini sio Irani au Korea ya Kaskazini? Ukimuuliza yule bwana wa Texas anayejifanya kuwa ni kma mtume Paulo, yaani katumwa na Yesu, Joji mwana wa Kichaka maswali haya atakwambia kuwa Marekani ina mfumo wa kidemokrasia kwahiyo ni sawa nchi hii ikiwa na silaha hizo ila nchi kama Korea ya Kaskazini na Irani zina madikteta vichaa ambao wanaweza kuanamiza dunia.

Mpige kofi na swali hili: Je sio Marekani hiyo unayodai kuwa ni nchi ya kidemokrasia ambayo ndio katika historia imetumia silaha mbaya kabisa dhidi ya raia ilipoangusha mabomu ya atomiki? Muulize hivi mfumo wa utawala wa Pakistani ni bora zaidi ya ule wa Irani? Maana unaona Pakistani ina silaha za nyuklia lakini Marekani imefunga domo. Ni kitu gani kinaipa Pakistani alama ya vema ya kuwa na silaha hizo ila sio Irani? Na kwanini zile nchi ambazo hazitaki kuwasikilizeni ndio ambazo hazina haki ya kuwa na silaha hizo ila nchi vibaraka wenu ndio zina haki hiyo?

Kwanza kwanini, bado umemkalisha Joji kiti moto, nchi yenu isiongoze vuguvugu la kidunia la kujenga dunia mpya isiyo na silaha za maagamizi hata kidogo? Na ukitaka kupata utamu wa majibu ya maswali haya usimruhusu Joji aulize wasaidizi wake majibu. Mwambie hakuna “kudesa.” Atoe majibu kichwani mwake mambo ya “kuangalizia” ni ya darasa la pili na la tatu!
Sijui ni lini Marekani itajifunza. Katika historia yake imetoa maamuzi mengi sana yenye madhara makubwa kwake na dunia nzima lakini haijifunzi. Walipokuwa wanakula sahani moja na akina Osama na jamaa wenye madevu wa Talibani walikuwa sijui wanafikiria nini. Ikaja Septemba 11, yaani 911 kama namba ya simu ya kuita manjagu hapa. Sasa tunaona yale madrasa yaliyojengwa na kuendeshwa na Matalibani yanamepeleka majonzi Uingereza. Kule Iraki ndio sijui wanafanya nini. Jana askari 14 wa Marekani wameuawa wakati Joji anadai kuwa nchi hiyo iko tayari kushughulikia suala la ulinzi na amani peke yake. Yaani wamekwenda kuibadili Iraki toka kuwa nchi hadi kuwa chuo cha mafunzo ya ugaidi. Nadhani Osama sasa anahamishahamisha vitu vyake kuelekea Iraki. Huko ndio hawa jamaa wanaona kuna utamu. Ndio jikoni.

Tuache hiyo, jinsi ambavyo siasa za Marekani zilitengeneza mazingira ya Talibani kutawala Afghanistani na kutumia sharia kali za kukata watu vichwa katika viwanja vya mpira...yaani kama watu wanavyokwenda uwanjani kumtazama Beckham akipiga krosi, kule Afghanistani watu walikuwa wanakwenda viwanjani kutazama watu wakikatwa vichwa. Sasa Iraki nako utawala kama wa Talibani umejitokeza kwenye miji kadhaa kama Basra. Na kwakuwa miji yenye utawala kama wa Talibani ina amani kiasi, Marekani imeamua kukaa kimya. Ifanyeje? Haijui cha kufanya.

Leo ni kati ya zile siku ambazo ninaanza kuandika jambo nikifika huku chini nakuwa nimesahau kuwa nilikuwa nataka hasa kusema nini. Na kwakuwa nina mambo kadhaa ya kufanya, sitaki kurudi kule juu kuanza kusoma upya. Nadhani mtanielewa ninasema nini.

0 Maoni Yako:

Post a Comment

<< Home

FREE hit counter and Internet traffic statistics from freestats.com