9/09/2005

Chakula cha hapa na mengineyo

Sisemi kwa ubaya. Ila sidhani kama rais wa Ufaransa, mzee Chirac, alikosea sana alipotoa mawazo yake mwezi wa saba mwaka huu juu ya chakula cha Kifini. Maneno yake yalikuwa makali kidogo. Jana wakati wa chakula cha usiku, mwandishi mmoja mwandamizi toka Afrika Kusini (amenisihi nisimtaje jina) aliniambia, "Kwetu bwana Macha ukila chakula hiki unakuwa ni sawa tu na mtu aliyelala njaa."
Nikamwambia, "Mbona?"
Akashangaa, "Yaani wewe huoni? Kwani hiki ni chakula? Unajua wajumbe toka India kila siku wanajipikia wenyewe kwa zamu kule jikoni."
Tuache chakula chao, Finland kama hufahamu ni nchi ambayo utenzi uliisaidia ikapata uhuru. Huu ni ule utenzi wa Kalevala. Mwaka 2000 nilishuhudia kundi la Parapanda likiigiza utenzi huu katika juma la makumbusho pale Dasalama. Kaiti ya mambo ambayo nchi hii inajivunia ni kazi za mchora ramani za majengo wa Kifini, Alvaro Aalto. Jengo la Finlandia Hall ambamo mkutano wa Helsinki unafanyika limechorwa na huyu bwana.
Katika mazungumzo na watu mbalimbali kumezuka mjadala kuhusu nchi za Afrika kusemekana kuwa ziko nyuma kimaendeleo kwakuwa zilitawaliwa. Swali hili limeulizwa: iweje Finland iliyotawaliwa karibu miaka 700 na Waswidi na miaka 150 na Warusi iwe mbele namna hii kiuchumi na kijamii?
Kwa mujibu wa Transparency International Corruption Perceptions Index Finland ndio nchi ambayo ina vitendo vichache kabisa vya rushwa. Na pia ndio nchi ambayo ina uchumi wenye ushindani mkubwa duniani kwa mujibu wa the World Economic Competetiveness Index.
Elimu na afya katika nchi hii hutoi hata sumni. Tofauti na nchi ya kibeberu kama Marekani, Finland hakuna shule au vyuo vikuu vya binafsi/kulipia.
Ingawa Finland ni nchi inayoelezewa kuwa tayari imeshaingia kwenye zama za jamii-habari, teknolojia ya blogu bado haijapokewa na wengi. Mmoja wa wanablogu wazuri hapa Finland ni Mmarekani mmoja mtalaamu wa mambo ya kompyuta.

0 Maoni Yako:

Post a Comment

<< Home

FREE hit counter and Internet traffic statistics from freestats.com